Monday 4 April 2016

FSC NA SHARP VICTOR ZATOSHANA NGUVU UWANJANI LEO


Timu za FSC ya Kangani na Sharp ya Micheweni leo zimegawana point baada ya kutoka sare ya kufungana magoli 3-3 kwenye mchezo wa ligi kuu ya Zanzibar kanda ya Pemba uliochezwa kwenye uwanja wa Gombani.

Mchezo huo ambao ulihudhuriwa na watazamaji wachache FSC ndiyo waliotangulia kujipatia bao katika dakika ya 5 lililofungwa na mchezaji wake Shahal Hassan ambaye alipachika la pili kwenye daki ya 19.

Hata hivyo kutangulia si kufika ndivyo ilivyotokea uwanjani hapo kwa Sharp Victor kuyarejesha mabao hayo kupitia kwa wachezaji wake Hamad Ali dakika ya 32 na Khatib Hamad katika dakika ya 39 na kulipeleka pambano hilo mapumziko timu hizo zikiwa zimefungana magoli 2-2.

Timu zote zilirudi kiwanjani katika kipindi cha pili kwa kasi huku FSC ikionekana kufuta makosa yake kwa kupanga mashambulizi ya uhakika, na ndipo kwenye dakika ya 67 walipojipatia goli la tatu lililofungwa na mchezaji Richard Gritan.

Dakika 2 kabla kumalizika kwa mchezo huo Sharp Victor ilifanikiwa kusawazisha goli la tatu lilowekwa wavuni na mchezaji wake Khamis Ali kwenye dakika ya 88.

Na hadi mwisho wa mchezo huo uliochezeshwa na mwamuzi Hassan Gerrei akisaidiwa na Suleiman Juma na Suleiman Kisauti FSC 3 na Sharp Victor.

Katika mchezo mwengine uliochezwa kwenye uwanja wa FFU Finya timu ya Jamhuri akaiadhibu Aljazira kwa magoli 4-1.

Katika mchezo wa kwanza Jamhuri ilikubali kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Chipukizi, huku Aljazira wakipokea kipigo cha magoli 4-1 kutoka kwa Kizimbani.


Kesho Jumanne kutakuwa na mchezo mmoja tu kwenye uwanja wa Gombani, mchezo unatabiriwa kuwa mkali kati ya Chipukizi na Kizimbani.

No comments: