Azam FC, leo Jumapili itarusha karata yake ya kwanza muhimu
kwenye raundi ya pili ya Kombe la Shirikisho Afrika, pale itakapowakaribisha
Esperance ya Tunisia katika Uwanja wa Azam Complex, jijini Dar es Salaam.
Azam itaingia dimbani ikiwa bila nyota wake wawili beki
Shomari Kapombe na kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’, ambao ni wagonjwa.
Kapombe bado yupo nchini Afrika Kusini akiendelea na vipimo
kwa ajili ya kubaini tatizo linalomsumbua kutokana na kubanwa mbavu huku Sure
Boy akisumbulia na mjeraha ya nyonga aliyoyapata wakati wa mchezo dhidi ya
Ndanda.
Akizungumza na mtandao wa www.azamfc.co.tz mara baada ya
mazoezi ya jana asubuhi Kocha Mkuu wa Azam FC, Stewart Hall, alisema licha ya
kuwakosa nyota wake hao amejipanga kutumia mfumo mpya utakaowawezesha kupata
matokeo ya ushindi dhidi ya Esperance.
“Nitawakosa Sure Boy na Kapombe kwenye mchezo dhidi ya
Esperance, Sure Boy anahitaji mapumziko ya siku nne ili kurejea kwenye hali
yake ya kawaida, kwa Kapombe bado haijajulikana kwani hivi sasa tunasubiria
ripoti kutoka Afrika Kusini kujua maendeleo ya afya yake.
“Nitakuja na mfumo mpya kwa ajili ya kupambana na hali hiyo
ambao utaanza tukiwa na mabeki wanne ambao utakuwa ni mzuri wa kupambana na
mfumo wa 4-2-3-1 wanaotmia wapinzani wetu, hivyo mabeki wa pembeni wataanza
Erasto Nyoni na Wazir Salum, pengo la Sure Boy litazibwa na Messi (Ramadhan
Singano), atakayecheza kama namba 10,” alisema.
Hall alisema amelenga ushindi kwenye mchezo huo na kudai kuwa
atapanga kikosi chenye muonekano wa kushambulia zaidi kwenye nafasi za mbele
ukiondoa viungo wawili wa ukabaji watakaokuwa wakiwasaidia mabeki kutimiza
majukumu ya kukaba.
Mfanano wa timu hizo
Timu hizo zinakutana wakati zikiwa na mfanano wa nafasi
katika ligi zao, wakati Azam FC ikiwa inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa
Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania kwa kujikusanyia jumla ya pointi 52, Esperance
nayo ipo nafasi hiyo ndani ya Ligi Kuu Tunisia baada ya kujizolea pointi 51.
Mpaka zinafikia raundi ya pili ya michuano hiyo, timu hizo
zimepenya raundi hiyo baada ya kupata ushindi mnono kwenye mechi za raundi ya
kwanza walipoanzia, Azam FC ikiitoa Bidvest Wits ya Afrika Kusini kwa jumla ya
mabao 7-3 huku Esperance nayo ikiifurusha nje Renaissance ya Chad kwa ushindi
wa 7-0.
Rekodi ya Azam FC (Azam Complex)
Azam FC bado ina rekodi nzuri kila inapotumia uwanja wake wa
nyumbani kwani mpaka sasa kwenye michuano yote ya kimataifa haijawahi kufungwa
ndani ya dimba hilo tokea waanze kuutumia kwa mechi hizo mwaka juzi.
Mabingwa hao wa michuano ya Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki
Kati (CECAFA Kagame Cup), walianza mwaka juzi kwa kuifunga Ferroviario de Beira
ya Msumbiji kwa bao 1-0 lililofungwa na Kipre Tchetche katika mchezo wa raundi
ya awali ya Kombe la Shirikisho, kabla ya kwenda kutolewa ugenini kwa kufungwa
2-0.
Mwaka jana ikawalaza vigogo wa Sudan, El Merreikh, kwa jumla
ya mabao 2-0 (Didier Kavumbagu, John Bocco) katika mchezo wa raundi ya kwanza
ya Ligi ya Mabingwa Afrika, lakini ikatolewa baada ya kupigwa 3-0 jijini
Khartoum, Sudan.
Mwaka huu ikailaza Bidvest Wits mabao 4-3 na kuvuka kwa
ushindi wa jumla ya mabao 7-3 kufuatia kuibuka na ushindi wa 3-0 katika Uwanja
wa Bidvest, jijini Johannesburg, hivyo kesho Azam FC itakuwa na kila sababu ya
kutaka kuendeleza rekodi yake hiyo bora.
Viingilio Azam FC v Esperance
Mashabiki wa soka nchini wamerahisisha kabisa kushuhudia
mchezo huo utakaokuwa mkali na wa aina yake, kwani ili uweze kushuhudia uhondo
huo itakugharimu kiasi kiduchu tu cha Sh. 5,000 kwa majukwaa ya mzunguko.
Kwa majukwaa ya watu maalumu (VIP), kiingilio cha VIP A
kitakuwa ni Sh. 20,000 tu huku VIP B kikiwa ni Sh. 10,000, ambapo tiketi zote
hizo zitapatikana siku ya mchezo (leo Jumapili) saa 3:00 asubuhi kwa kuuzwa
kwenye Ukumbi wa Dar Live Mbagala Rangi Tatu na kituo kingine kitakuwa katika
Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam itakapofanyika mechi hiyo.
chanzo:Shaffih Dauda
No comments:
Post a Comment