Friday 1 April 2016

JAMHURI YALALA NA MACHOFU LEO HII


Na Is-haq Muhammed Salma Sport's media


Timu ya Chipukizi imeianza vyema ligi kuu ya Zanzibar baada ya leo kuinyuka wakongwe wenzao wa soka kisiwani Pemba na Zanzibar kwa ujumla timu ya Jamhuri kwa bao 1-0.

Alikuwa ni mchezaji wa zamani wa timu ya Simba ya jijini Dar-es salaam Soud Abdalla aliyezitikisha nyavu za Jamhuri  jua ikiwa limeshazama katika dakika ya 84.

Katika mchezo ambao ulikuwa wa ushindani mkubwa timu ya Chipukizi ilionekana kulielemea zaidi lango la Jamhuri hasa katika kipindi cha kwanza na kama wachezaji Faki Khamis na Rashid Moh`d wangalikuwa makini wengepeleka madhara mapema langoni mwa wapinzani wao.

Hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika hakukuwa na timu iliyoweza kulifuma lango la mwenzake.

Hata hivyo Jamhuri haitaacha kuwalaumu washambuliaji wake akiwemo Abdalla Othman kutokana na kushindwa kuzitumia nafasi chache walizozipata katika dakika za 57, 67 na 81.

Akizungumzia SALMA SPORT’S MEDIA juu ya kupoteza mchezo huo kocha wa Jamhuri Ameir  Chua amesema ni makosa yaliyofanywa na walinzi wake ndiyo yaliyotoa nafasi kwa wapinzani wao kuwafunga bao hilo, huku akiahidi kufanya vyema katika michezo ijayo.

Kocha Mzee Ali Abdalla wa Chipukizi amesema mchezo ulikuwa mkali sana, hata hivyo amesema juhudi zilizofanywa na wachezaji wake zimeweza kuivusha timu hiyo katika mchezo huo kwa kupata alama 3 muhimu.

Aidha Mzee amesema timu ya Jamhuri sio ya kubeza kutokana na kiwango kikubwa walichokionyesha katika mchezo huo.

Katika mchezo mwengine wa ligi kuu ya Zanzibari kanda ya Pemba uliochezwa leo kwenye uwanja wa FFU Finya timu ya Kizimbani imeiadhibu vibaya timu ya Aljazira kwa kuipiga mabao 4-2.

Timu ya Young Islanders nayo ikaondoka patupu kwa kupokea kipigo cha magoli 2-1 kutoka kwa African Kivumbi katika mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Kangani Skuli.


Ligi kuu ya Zanzibar Kanda ya Pemba itaendelea tena kesho kwa timu ya Dogo Moro kuwaakaribisha Mwenge katika uwanja wa Gombani, ambapo huko FFU Finya Okapi wataikaaribisha Madungu.

No comments: