Wednesday 9 March 2016

Madrid Yafuzu Huku Ronaldo akiifukuzia kuvunja rekodi yake mwenyewe ya Magoli UCL

Real Madrid hatimaye wamefanikiwa kuingia kwenye hatua ya robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa wa ulaya kwa mara ya sita mfululizo baada ya kuiondoa AS Roma kwenye raundi ya 16 bora.
Katika kufanikisha hatua hiyo Cristiano Ronaldo alikuwa kwenye mission mbili – kuivusha timu yake na kuifukuzia rekodi mpya  ya ufungaji  katika Champions League.
  Nahodha huyo wa Ureno aliifungia Real Madrid goli la kuongoza usiku wa jumanne dhidi ya AS Roma likiwa goli lake la 90 kwenye michuano hiyo, kabla ya kutoa assist kwa James Rodriguez katika kuhakikisha timu yake inafuzu kwenda hatua ya robo fainali ya michuano ya ulaya – Los Blancos wakifuzu kwa ushindi wa jumla wa 4-0.
Kwa goli lake vs AS Roma, CR7 ametimiza magoli 13 katika michuano ya ulaya msimu huu,  na kuacha magoli manne tu kuifikia rekodi ya kuwa mchezaji aliyefunga magoli mengi zaidi katika msimu mmoja wa UCL – alifunga magoli 17 msimu ambao Madrid walitwaa La Decima 2013-14.
  Baada ya Los Blancos kufanikiwa kuingia robo fainali – sasa kuna uwezekano Ronaldo akapata mechi mbili zaidi za kuifikia na kuivunja rekodi aliyoiweka misimu kadhaa iliyopita.
Na idadi ya magoli 27 aliyonayo mshambuliaji huyo kwenye La Liga na moja alilofunga leo dhidi ya AS Roma – inamaanisha kwamba Ronaldo sasa ametimiza magoli 40, idadi ambayo amekuwa akiivuka kila msimu katika kipindi cha miaka 6 iliyopita.
  Katika hatua nyingine Wolfsburg wamefanikiwa kufuzu kwenda robo fainali baada ya kupata ushindi wa jumla ya 4-2 dhidi ya Gent.
 
Shaffih Dauda.

No comments: