Sunday 28 February 2016

RONALDO AWAPIGA DONGO WACHEAJI WA MADRID BAADA YA KIPIGO CHA ATLETICO


Cristiano Ronaldo amewashukia wachezaji wenzake wa Real Madrid baada ya kipigo cha jana kutoka kwa mahasimu wao Atletico Madrid, akidai kwamba Madrid wangeweza kuwa kileleni mwa ligi endapo tu wachezaji wenzake wangekuwa na kiwango kama cha kwake.
Goli pekee la Antoine Griezmann katika kipindi cha pili lilitosha kuwapa Atletico ushindi wa 1-0 ugenini na kuwaacha wapinzani wao pointi tisa nyuma ya vinara wa Liga Barcelona, ambao hata hivyo wana mchezo mmoja mkononi.
Akifanyiwa mahojiano baada ya mchezo huo, Ronaldo aliwalaumu wachezaji wenzake kama ndiyo sababu za kutofanya vizuri kwa timu yao huku pia akitupilia mbali tuhuma za kwamba yeye ndiye chanzo cha matokeo mabovu  ya timu hiyo.
“Kama kila mtu angekuwa vizuri kama mimi, pengine tungekuwa kileleni kwa sasa,” alisema.
“Simaanishi kwamba nawashusha ila maana yangu ni kwamba wakiwa hawapo kwenye ubora wao ni vigumu sana kupata matokeo. Napenda sana kucheza na Karim, Bale na Marcelo.
“Sina maana ya kwamba Jese, Lucas [Vazquez] na [Mateo] Kovacic sio wazuri, hapana, ni wazuri lakini, ili kushinda kwenye mechi yenye ushindani mnahitaji kuwa bora na hicho ndicho kilichokosekana msimu huu.
“Sasa sifahamu kama sababu ni maandalizi mabovu ya mwanzo wa msimu lakini majeraha mengine yanayowakabili wachezaji inawezekana ndiyo sababu kubwa pia.
“Kutokana na kinachoongelewa kwenye vyombo vya habari, inaonekana kana kwamba mimi ndiyo nafanya madudu lakini ukweli ni kwamba namba na takwimu mara zote hazidanganyi .”
shaffih dauda

No comments: