Tuesday 23 February 2016

SIMBA SC HAWANA CHA KUJITETEA, JONESIA WEWE NI BONGE LA MWAMUZI

Nimegundua kuwa katika mpira wa miguu Tanzania mwamuzi mzuri huonekana mbaya pale tu anaposimamia vizuri sheria za mchezo wenyewe na kuzitolea maamuzi sahihi. Baada ya mwanadada Jonesia Rukyaa kumlamba kadi nyekundu mlinzi wa Simba SC, Abdi Banda katika dakika ya 25 ya mchezo waliopoteza 2-0 dhidi ya mahasimu wao Yanga SC.
Lawama zote za kupoteza mchezo ‘Wana-Simba’ wameelekeza kwa mwamuzi huyo kwa madai kwamba alipaswa kwanza kumuonya Banda kabla hajamwonyesha kadi ya kwanza ya manjano kwa kosa la kumchezea faulo mshambulizi wa Yanga, Donald Ngoma. Lakini ni sababu za ‘mfa maji,’ ambaye haishi kutapatapa wakati akiangamia.
Jonesia alikuwa imara na alikimbia kila mpira ulipokwenda. Alifanya vizuri kumpa kadi ya kwanza ya njano kwa Banda baada ya mchezaji huyo kumuonesha dharau. Alijitengenezea sura ya nidhamu. Akasimamia vizuri uamuzi wake wa kumpa kadi ya pili ya njano. Hakika mwanadada huyu ni shupavu.
Ni mwamuzi aliyeimudu mechi na hakuwa na presha wala hakuwa muoga wa kelele za mashabiki wa Simba. Ni bonge la mwamuzi kwa hakika, japo wengine watapinga.  Simba hawana cha kujitetea zaidi makosa yao wenyewe ndiyo yalifungua njia za Yanga kukamilisha ushindi wao.
Simba ilistahili kupoteza mechi ya pili mfululizo mbele ya mahasimu wao tangu mwaka 1999. Takribani miaka 16 mfululizo iliyopita Yanga haikuwahi kuwafunga Simba katika michezo yote miwili katika msimu mmoja wa ligi kuu Tanzania Bara.
KADI YA PILI YA NJANO YA ABDI BANDA
Ilikuwa ni faulo ya pili kuchezwa na Banda . Banda lilikuwa chaguo zuri sana katika ngome ya Simba, hadi dakika 20 za kwanza Yanga haikuwa imefanya shambulizi lolote lile la kutisha katika lango la Simba, na tayari walikuwa wamecheza mipira mingi ya kona iliyoelekezwa langoni kwao.
Licha ya kwamba Simba walishambulia mfululizo bila kuchoka kwa dakika zaidi ya 20 za mwanzo. Ukuta wa Yanga haukupoteza umakini wala nidhamu yao ya mchezo. Nafikiri kwa wiki nzima kuelekea mchezo huo wa siku ya jana Jumapili, kikosi cha kocha Mganda, Jackson Mayanja kilikuwa kimewekeza katika mpango wa kushambulia na kuhakikisha kuwa wanapata goli la kuongoza ndani ya dakika 15 za kwanza.
Mtogo, Vicent Bossou alicheza na mlinzi mwingine Mnyarwanda, Mbuyu Twite kama walinzi wa kati-namba 4-na namba 5, na mbele yao akapangwa kijana Pato Ngonyani. Wachezaji hao watatu walicheza kwa nidhamu ya hali ya juu licha ya kupokea mashambulizi mengi. Hivyohivyo ndivyo walicheza walinzi wa pembeni, Juma Abdul na Mwinyi Hajji.
Walitengeneza ugumu ambao isingewezekana kwa mastraika wa Simba kupata nafasi za wazi. Katika hali ya kaiwaida, ndani ya dakika 45 za kila kipindi cha mchezo huwa kuna ‘vipindi vitatu,’ dakika 15 za kushambulia, dakika 15 za kupokea mashambulizi na dakika nyingine 15 za kupumzika.
Yanga walikuwa wa kwanza kufika upande wa goli la Simba kwa jaribio la Ngoma dakika ya kwanza tu ya mchezo, lakini mpira walipoupata Simba hakika walikuwa na dakika 15 ngumu lakini wakastahimili presha na wakati wakiingia katika dakika 15 za pili kwa lengo la kupumzika na kupunguza presha ya mashambulizi ya Simba wakaanza kupiga mipira kwenda mbele kwa kuamini uwepo wa Ngoma na Deus Kaseke na uwezo wao wa kuhifadhi mpira ungewasaidia.
Baada ya Banda kuoneshwa kadi ya njano ya kwanza, ambayo naweza kusema alijitakia Yanga wakagundua kuwa nidhamu ya kimchezo ya Simba ipo chini na uwepo wa wachezaji wao 6 wa kimataifa uliwasaidia haraka kuubadilisha mchezo uliokuwa mgumu upande wao kuwa rahisi.
Kadi ile ya njano ya kwanza, Banda alijitakia kwa maana alionekana kumdharau mwamuzi wakati alipomwita,  nafikiri angepewa onyo tu la kawaida kwa kuwa ilikuwa ni faulo yake ya kwanza katika mchezo tena haikuwa ya kutisha.
Ila alikuwa na kiburi. Na kama angejua kilichokuwa mbele yake dakika 3 baadaye bila shaka angemnyenyekea mwamuzi wakati alipofanya faulo isiyostahili kadi. Kadi ya pili ya manjano alipata dakika ya 25 na ikafuata kadi nyekundu. Nini kilifuata? Aliimaliza timu yake, akamaliza mbinu zote za Mayanja, akaondoa hali ya kujiamini katika timu yake na mwisho wa mechi ilionekana pengo lake kwa dakika 65 liliwachosha wenzake.
PASI MKAA YA KESSY 
Katika uchambuzi wangu kabla ya mechi nilisema kwamba Simba huwa wanakawaida ya kupotezakupoteza sana pasi.  Kwa maana fupi ni kuwa pasi zao nyingi hupotea na niliweka wazi kuwa wataadhibiwa kwa tatizo hilo kama hawatajirekebisha.
Licha ya kwamba walikuwa pungufu kwa mchezaji mmoja uwanjani, Simba walijaribu mara kadhaa kuendelea kushambulia goli la Yanga lakini wakashindwa kuipenya ngome ngumu iliyokuwa chini ya nahodha, Bossou.
Wakati walinzi wa Yanga walicheza kwa umakini muda wote, Hassan Kessy ambaye alipangwa kama beki 2 wa Simba alifanya kosa la pili kubwa upande wa timu yake. Katika mazingira yasiyotarajiwa na wengi mlinzi huyo aligeuka upande wake na kurudisha pasi-mkaa kwa golikipa wake Mu-ivory Coast, Vicent Angban. Pasi hiyo iliwahiwa na straika Ngoma naye akamlamba chenga rahisi kipa huyo na kufunga goli la kuongoza upande wa timu yake.
Alichopaswa kufanya Kessy kama hakukuwa na mazingira rahisi ya kuupeleka mpira mbele, angeutoa tu na kuwa kona ili wajipange kuzuia. Kosa lake lilielekea kuimaliza zaidi Simba na kuwafanya wapoteze kabisa matumaini ya kupata ushindi.
SUB YA MWINYI KUMPISHA NOVATUS LUFUNGA
Yanga ilipanga walinzi watano, viungo watatu na straika wawili, wakati Simba iliwapanga viungo wanne, walinzi wanne na straika wawili. Kama kadi nyekundu ya Banda dakika ya 25, Simba walikuwa bora katikati ya uwanja lakini baadaye wakaanza kuzidiwa. Mzimbabwe, Justice Majabvi ilibidi arudishwe nyuma kabisa kucheza beki ya kati sambamba na Mganda, Juuko Murishid.
Nahodha, Jonas Mkude akarudi chini katika kiungo namba 6 na kuwaacha Said Ndemla na Mwinyi Kazimoto wakipanga mashambulizi. Kabla ya goli la ‘kujitakia’ walilofungwa Simba dakika ya 39, viungo wa Yanga hawakuonekana kuwa na madhara sana lakini kitendo cha kupungua kwa mchezaji mmoja wa Simba kiliwafanya, Kaseke, Thaban Kamusoko na Haruna Niyonzima kuanza kwenda mbele.
Nilishangazwa na mabadiliko ya kutoka kwa Kazimoto na kuingia mlinzi wa kati, Novatus Lufunga kwa kuwa tayari Majabvi alikuwa na uwezo wa kubeba majukumu ya beki wa kati. Kwa dakika zaidi ya 20 alicheza kama beki wa kati na alifanya vizuri.
Nafikiri, sub-ya kwanza ya Simba ilikuwa ni kumtoa Hamis Kizza na kuingia Brian Majwega ambaye alikuja kupewa nafasi dakika kumi za mwisho. Uwepo wa Mkude, Ndemla, Kazimoto na Majwega katika kiungo kungemaanisha, Ibrahim Ajib angebaki kama mshambuliaji pekee mbele. Asingefanya lolote lakini ingesaidia Simba kucheza vizuri licha ya kwamba walikuwa pungufu.
Majwega ana uwezo wa kujibadilisha uwanjani na kucheza kama mshambuliaji pia ni mchezaji ambaye angesaidia sana katika umiliki wa mpira na kuwa namba ya ziada pia kwa safu ya kiungo. Kuendelea kumuacha uwanjani Kizza aliyeonekana kuikamia mechi na kumtoa Kazimoto ilikuwa sub mbaya na ilichangia kipigo cha Simba.
PATO NGONYANI, BOSSOU NA TWITE
Simba walichukulia kutokuwepo kwa walinzi Kelvin Yondan na Nadir Haroub katika ngome ya Yanga kungewayumbisha timu hiyo lakini alichokifanya kocha M-holland, Hans Van der Pluijm ni kuwajaza walinzi wengi wa kati ili kuhakikisha washambuliaji Kizza na Ajib hawapati nafasi ya kuwa peke yao mchezoni.
Walinzi hawa watatu wa Yanga walikuwa sababu kubwa ya ushindi wa Yanga licha ya kwamba washambuliaji Ngoma na Tambwe walifunga magoli makali ya kujitolea. Simba walishindwa kabisa kuupita ukuta huu wa watu watatu.
Sasa inamaanisha katika gemu 8 zilizopita za VPL zilizowakutanisha ‘mahasimu’ Yanga SC v Simba SC, ‘Wekundu wa Msimbazi’ wamefanikiwa kushinda mechi 1 tu. Nachokumbuka kuhusu Simba ya zamani ni kwamba ilikuwa na uwezo wa kuifunga Yanga hata pale walipokuwa pungufu uwanjani lakini Simba hii ya sasa ikibaki pungufu tu jua imekwisha.
shaffih dauda.

No comments: