Wednesday 30 March 2016

WAWI STAR KUKIPIGA LIGI KUU YA ZANZIBAR MWAKANI.



Jezi rangi ya Njano ni timu ya Wawi Star wakati  Mwamuzi Mwadini Ali akimsikiliza mlinzi wa timu hiyo.

Timu ya Wawi Star yanyakuwa ubingwa wa ligi daraja la Kwanza Taifa Pemba baada ya jana kufanikiwa kuichapa timu ya Dangers Boys magoli 2-1 katika mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Gombani.

Timu ya Wawi Star inakuwa bingwa ikiwa imebakiwa na mchezo mmoja mkononi baada ya kucheza michezo minne na kushinda mitatu na kutoka sare mchezo mmoja.

Kutokana na ushindi huo wa jana uliowahakikishia kucheza ligi kuu ya Zanzibar kanda ya Pemba msimu ujao, mashabiki wa Wawi Star walilazimika kufanya shangwe na vifijo huku wakiondoka uwanja wa Gombani kwa kidedea hadi walipofika katika makazi yao huko Wawi.

Timu ya Wawi Star katika hatua ya makundi ambapo ilikuwa kundi la kusini Pemba ilishika nafasi ya pili kwa kupata alama 33, nyuma ya mahasimu wao Mkungu Malofa waliofikisha alama 34.

Katika hatua ya 6 Bora Wawi imejipatia jumla ya alama 10, ikifiatiwa na Chuo/Basra yenye alama 6, Mkungu Malofa 5, Dangers Boys 4, Maji maji 4 na New Star 4.

Mchezo unaotarajiwa kuchezwa leo katika ya timu ya Mkungu Malofa na Maji maji huenda ukatoa timu nyengine itakayopanda daraja, huku timu nyingine zikijulikana hapo kesho baada ya mchezo kati ya Chuo/Basra yenya alama 6 na Maji maji yenye alama 4, na mchezo baina ya Timu ya Wawi Star na New Star ambayo nayo inajipa moyo wa kupata nafasi hizo.

Timu 3 za juu zilizoingia katika hatua ya 6 ndizo zitakazopanda daraja kucheza ligi kuu ya Zanzibar msimu ujao.

No comments: